Skip to main content

UKWELI KUHUSU P2

p2 ni nini? 

"Morning pills" ama "p2" kama zinavyofahamika na watu wengi mtaani, ni dawa za dharura zinazotumika kuzuia mimba. p2 zina homoni inayoitwa "levenogesterol" ambayo hufanya kazi ya kuzuia mimba kwa njia kuu tatu: 

  • Huzuia yai kutolewa (Ovulation)
  • Huzuia mbegu ya kiume kukutana na yai (Fertilization)
  • Huzuia yai lililotungwa kujishikiza kwenye mji wa uzazi (Implantation) 

Dawa hizi ni kwa ajili ya dharura tu, na hufanya kazi ndani ya masaa 72 baada ya kufanya tendo ka ndoa bila kinga, ufanisi wake unaweza kufika hadi asilimia 95 ikiwa zitatumika mapema. 

Mara ngapi nitumie p2?

Ni salama kutumia p2 mara moja katika mzunguko mmoja wa hedhi, matumizi ya mara nyingi ndani ya mzunguko mmoja wa hedhi yanaweza kusababisha madhara makubwa zaidi ya homoni na mzunguko wa hedhi. 
Matumizi ya mara kwa mara yanaweza kusababisha mzunguko wa hedhi usio tabirika, kutokuwepo kwa hedhi kwa muda mrefu, au kutokwa na damu isiyo kawaida (spotting). 

p2 zinabeba dozi kubwa ya homoni (levenogesterol) ambayo inaweza kuvuruga mzunguko wa kawaida wa homoni mwilini. Hii inaweza kusababisha kubadilika kwa hedhi, maumivu ya kichwa na hisia za kuchoka au kukosa nguvu. 

p2 inaweza kusababisha utasa?

Hapana! Matumizi ya p2 yanaweza kusababisha madiliko ya mzunguko wa hedhi au kutokuwepo kwa hedhi kwa muda, lakini hayaathiri uzazi wa muda mrefu. Uwezo wa kupata mimba utarejea mara tu baada ya mzunguko wa hedhi kurudi.

p2 inaweza kusababisha saratani?

Hakuna ushahidi wa moja kwa moja unaoonesha dawa hizi zina uhusiano na saratani ya ovari, matiti, shingo ya kizazi au mfuko wa kizazi. 
Homoni iliyomo kwenye dawa za p2 ni sawa na iliyomo kwenye dawa za uzazi wa mpango (COC), ingawa matumizi ya muda mrefu (miaka mitano au zaidi) ya COC yanahusishwa na kuongezeka hatari ya kupata saratani ya matiti au saratani ya shingo ya kizazi, kwa p2 kwasababu matumizi yake ni ya muda mfupi, hayajatajwa kuongeza hatari ya saratani ya aina yoyote. 

p2 inaweza kusababisha mimba ya nje ya mfuko wa uzazi (ectopic pregnancy)?

Ndiyo, matumizi ya p2 ikiwa ovulation tayari imefanyika na yai limekwisha rutubishwa inaongeza uwezekano wa yai lililorutubishwa kujipandikiza sehemu isiyo sahihi, mara nyingi kwenye mirija ya falopia. 
Ingawa hatari ya ectopic pregnancy si kubwa, ni muhimu kutumia p2 kwa uangalifu na kwa kufuata ushauri wa daktari ikiwa unahisi dalili zisizo za kawaida baada ya kutumia. 

p2 inaweza kusababisha mimba kutoka au mtoto kufia tumboni?

Hakuna ushahidi wa kisayansi unathibitisha moja kwa moja kwamba p2 inaongeza hatari za mimba kutoka (miscarriage) au mtoto kufia tumboni (still birth), ikiwa p2 imetumika tayari kuna ujauzito haina uwezo wa kuharibu mimba. 

Kwa kumalizia, p2 ni suluhisho la dharura kwa kuzuia mimba, lakini inapaswa kutumika kwa uangalifu na si kama njia ya mara kwa mara ya uzazi wa mpango. Ingawa haina madhara ya muda mrefu kama utasa au kuongeza hatari ya saratani, matumizi yake yanapaswa kuwa ya kipekee katika hali za dharura. Ni muhimu kushauriana na mtaalamu wa afya kabla ya kutumia ili kuhakikisha inatumika kwa usahihi na kuepuka athari zisizohitajika. Afya yako ni kipaumbele, hivyo chagua njia bora na salama ya uzazi wa mpango kwa maisha ya afya na utulivu.


Comments